Shirika la Sea Sense limetoa mafunzo maalum juu ya uwasilishaji wa takwimu kupitia mfumo wa kidigitali wa ukusanyaji Takwimu (Kobo Collect) kwa Wakusanya Takwimu katika Vikundi vya Usimamizi wa Rasilimali za Bahari (BMU) kutoka Kilwa Kusini. Mafunzo hayo yamefanyika katika Ukumbi wa Chuo cha Maendeleo ya Wananchi (FDC) Kilwa Kuanzia Tarehe 13 hadi 15 May 2025.
Lengo kuu la Mafunzo hayo ni kuwezesha upatikanaji wa taarifa sahihi na za kweli kuhusu rasilimali za bahari, ili kusaidia kuongeza mapato ya Halmashauri na taifa kwa ujumla. Kupitia matumizi ya mfumo wa kidigitali, wakusanya takwimu wataweza kurahisisha ukusanyaji na utoaji wa taarifa muhimu zinazohusiana na shughuli za uvuvi na matumizi ya rasilimali za bahari.
Akitoa mafunzo hayo, Afisa Ufuatiliaji,Tathmini na Mafunzo kutoka Sea Sense, Ndg. Ambonisye Haule, amesisitiza washiriki kutumia vyema elimu waliyoipata katika kutunza na kuwasilisha takwimu sahihi ambapo ameeleza kuwa taarifa sahihi ni msingi muhimu wa kupanga na kutekeleza sera bora za usimamizi wa rasilimali za bahari.
“Tunatarajia kuona mabadiliko chanya kupitia matumizi ya mfumo huu wa kidigitali katika ukusanyaji wa takwimu. Hii itasaidia kuongeza uwazi, uwajibikaji na hatimaye kukuza uchumi wa jamii na taifa,” amesema Ndg.Haule.
Kadhalika Afisa Uvuvi Wilaya ya Kilwa Ndg. Ulimboka Ndile amelipongeza Shirika la Sea Sense kwa kuandaa mafunzo hayo ambayo yataenda kusaidia kuongeza mapato na kuleta maendeleo katika Sekta ya Uvuvi hususani katika kutunza na kulinda rasilimali za Bahari.
Moja ya Washiriki katika Mafunzo hayo Bw. Hassan Mtalika ametoa shukrani kwa Shirika la Sea Sense juu ya Mafunzo ya uwasilishaji wa Takwimu kidigitali kwani hii itaenda kuwasaidia katika kuondoa Changamoto za uwasilishaji wa taarifa zao ikiwemo umbali na kupunuza gharama za kutumia makaratsi kama ilivyokuwa hapo awali.
Kilwa Masoko
Anuani ya Posta: 160
Simu: 0672365354
Simu: 0672581557
Barua pepe: ded@kilwadc.go.tz /ictsupport@kilwadc.go.tz
Hatimiliki@2017 Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa