Mkuu wa Wilaya ya Kilwa Mhe.Mohamed Nyundo, amewataka wavuvi Wilayani Kilwa kuachana na uvuvi haramu unaoweza kuhatarisha kuongezeka kwa rasilimali za Bahari ikiwemo Samaki ili kusaidia kukua kwa uchumi na ustawi katika ya Sekta ya Uvuvi Wilayani Kilwa.
Kikao hicho kimefanyika tarehe 09/05/2025 katika Ukumbi wa Chuo cha Maendeleo ya Wananchi (FDC) Kilwa, ambapo mhe. Nyundo amezungumza na Viongozi wa BMU na kujadili juu ya kutafuta suluhisho la kudumu kwa matatizo sugu ya uvamizi kwenye maeneo ya miamba darasa pamoja na uvuvi haramu unaoathiri ustawi wa mazingira ya baharini na kipato cha wavuvi halali.
Akizungumza na viongozi wa BMU, Mhe. Nyundo amesisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya serikali na wadau wa sekta ya uvuvi katika kulinda rasilimali za bahari na kuhakikisha kuwa shughuli za uvuvi zinaendeshwa kwa mujibu wa sheria.
“Tunapaswa kushirikiana kwa karibu kuhakikisha kuwa tunatokomeza uvuvi haramu na uvamizi kwenye maeneo ya hifadhi ya bahari, hii ni kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho,” amesema Mhe. Nyundo.
Viongozi wa BMU waliwasilisha mapendekezo mbalimbali ikiwemo kuimarishwa kwa doria, elimu kwa jamii kuhusu madhara ya uvuvi haramu, pamoja na kushirikishwa zaidi katika maamuzi ya usimamizi wa rasilimali za bahari.
Kikao hicho ni sehemu ya jitihada za serikali ya Wilaya ya Kilwa katika kuimarisha usimamizi wa fukwe na kuendeleza uvuvi endelevu unaozingatia utunzaji wa mazingira.
Kilwa Masoko
Anuani ya Posta: 160
Simu: 0672365354
Simu: 0672581557
Barua pepe: ded@kilwadc.go.tz /ictsupport@kilwadc.go.tz
Hatimiliki@2017 Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa