Katika kuadhimisha Siku ya Nyuki Duniani Tarehe 20 Mei, ya kila mwaka, Wilaya ya Kilwa imeungana na dunia nzima kwa kuendesha mafunzo ya siku mbili kwa wanachama wa kikundi cha uhifadhi wa mikoko (UWAMIKO) kilichopo Kilwa Masoko. Maadhimisho hayo yamefanyika kwa lengo la kuongeza uelewa juu ya ufugaji wa nyuki kama sehemu ya juhudi za kuhifadhi mazingira na kuongeza kipato kwa wananchi.
Siku ya kwanza ya maadhimisho ambayo ni tarehe 19 Mei, 2025 ilihusisha semina ya kitaalamu juu ya ufugaji wa nyuki ambapo jumla ya washiriki 25 kutoka kikundi cha UWAMIKO walipata nafasi ya kujifunza mbinu bora za ufugaji wa kisasa, faida za nyuki katika mazingira, pamoja na fursa za kiuchumi zinazopatikana kupitia bidhaa za nyuki.
Siku ya pili ambayo ndio siku ya kilele cha maadhimisho iliangazia utekelezaji kwa vitendo kupitia utundikaji wa mizinga ya nyuki katika maeneo ya hifadhi ya mikoko. Zoezi hilo lililenga kuwawezesha washiriki kutumia kwa vitendo maarifa waliyopata na kuanza hatua za awali za ufugaji wa nyuki katika mazingira yao.
Maadhimisho haya yameonesha namna jitihada za kijamii na za mazingira zinavyoweza kuunganishwa kwa njia endelevu. Kupitia ushirikiano kati ya wananchi na wadau wa maendeleo, Wilaya ya Kilwa inaendelea kuhamasisha shughuli za kiuchumi zinazolinda mazingira na kuchangia katika maisha bora ya wananchi wake.
Kilwa Masoko
Anuani ya Posta: 160
Simu: 0672365354
Simu: 0672581557
Barua pepe: ded@kilwadc.go.tz /ictsupport@kilwadc.go.tz
Hatimiliki@2017 Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa